
Katika mazingira ya ukandamizaji unaoongezeka, mpinzani wa Uganda Bobi Wine na mke wake wanaishi mafichoni. Mkinzano wa utawala wa Museveni unaonyesha udhaifu wa uhuru wa kisiasa barani Afrika, ambako mara nyingi upinzani hunyamazishwa kwa nguvu.
Ujumbe uliowekwa kisha kufutwa na mshirika wa karibu wa rais Yoweri Museveni, uliodai kifo cha Bobi Wine, umefufua hofu kuhusu kiongozi wa upinzani wa Uganda.
Muda mfupi baadaye, vikosi vya usalama vilizingira makazi yake, operesheni ambayo waziri wa Habari, Chris Baryomunsi, aliitetea akisema Bobi Wine «hana sababu yoyote ya kujificha».
Kwa mujibu wa Baryomunsi, uangalizi huo ulikuwa na lengo la kudhibiti «kuingia na kutoka» katika makazi ya mpinzani huyo. Lakini kwa upinzani, hii ni mbinu ya vitisho.
Akizungumza na waandishi wa RFI, Joel Ssenyonyi, msemaji wa NUP, alilaani «mateso» na kutaja kauli rasmi kuwa «hazina msingi».
Anaituhumu jeshi kwa kuvamia nyumba ya Bobi Wine, kumshambulia mke wake na kuiba mali. «Upande mmoja wanasema hayupo kwenye orodha ya wanaosakwa, na upande mwingine wanaendesha operesheni ya kikatili», alisisitiza.
Muhoozi Kainerugaba, mwana wa rais na mkuu wa jeshi, naye ameongeza mkanganyiko. Baada ya kukanusha uwepo wa msako, alikiri kwamba Bobi Wine anasakwa, huku akikataa tuhuma za mashambulizi.
Muhoozi huyo huyo anatuhumiwa na upinzani kwa kutishia mara kadhaa maisha ya Bobi Wine, hata kufikia hatua ya kutaja uwezekano wa kumuondoa. Kauli hizo zinaimarisha hali ya hofu inayomzunguka wanandoa hao.
Kwa zaidi ya miaka arobaini, Yoweri Museveni ametawala Uganda kwa mkono wa chuma. Utawala wake unatuhumiwa kwa kukandamiza upinzani mara kwa mara, kuwafunga au kuwaondoa wapinzani wake, huku ukidai ushindi mkubwa wa uchaguzi.
Kwa Joel Ssenyonyi, mkakati huu unaonyesha mkanganyiko: «Iwapo mna umaarufu mkubwa, kwa nini mnaendelea kuwatesa wapinzani wenu?» alihoji kwa RFI. Swali hili linazidi mipaka ya Uganda na kuonyesha udhaifu wa upinzani barani Afrika, mara nyingi ukandamizwa na tawala za kiimla.
Emmanuel Bin Vikingi