
Hali ya usalama inaendelea kuwa ya kutia wasiwasi katika wilaya ya Mambasa, mkoani Ituri, ambapo watu wasiopungua tisa wanadaiwa kutekwa nyara ndani ya kipindi cha siku mbili katika maeneo ya Makumo na Mantumbi, kwa mujibu wa Chama cha Kulinda Haki za Watoto na Wanawake Walio katika Mazingira Hatarishi (APDEF).
Kwa mujibu wa mratibu wa APDEF katika wilaya ya Mambasa, Ram’s Malikidogo, watu watatu, akiwemo baba mmoja na watoto wake wawili, wanadaiwa kutekwa nyara katika kijiji cha Kalongo, karibu na Mantumbi, kufuatia shambulio lililotokea Jumatatu, tarehe 27 Julai 2026, huko Makumo. Raia wengine sita pia wanadaiwa kuchukuliwa mateka Jumanne, tarehe 28 Julai 2026, katika kijiji cha Nakota.
APDEF inawahusisha waasi wanaodaiwa kuwa wa kundi la ADF na matukio hayo ya utekaji, likieleza kuwa kundi hilo linaendelea kufanya shughuli zake katika sehemu hiyo ya wilaya ya Mambasa. Shirika hilo limeeleza wasiwasi mkubwa kuhusu kuongezeka kwa hali ya ukosefu wa usalama na vitisho vinavyowakabili raia.
Kutokana na hali hiyo, APDEF imewataka wakazi wa maeneo ya Mabuho, Kalalangwe, Maleki, Beu, Musangwa na Mamove kuwa waangalifu zaidi. Pia limewasihi kutoa taarifa haraka kwa vyombo vya usalama kuhusu mienendo yoyote inayotia shaka ili kusaidia kuzuia mashambulizi mengine.
Hadi sasa, mamlaka za usalama hazijatoa taarifa rasmi kuthibitisha matukio hayo ya utekaji wala kueleza hatua zinazochukuliwa kuwatafuta watu wanaodaiwa kutoweka.
Obady Madirisha