
Wakulima wa maeneo ya Mikuha Kididiwe, iliyoko katika vijiji vya Bapakombe-Bakondo, wilaya ya Beni (Kivu Kaskazini), wamelalamikia vitendo vya unyanyasaji ambavyo wanavihusisha na wapiganaji wa Wazalendo wanaofanya shughuli katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa wakazi kadhaa waliowasiliana na mwana ripota wetu,wapiganaji hao waliwalazimisha wananchi siku ya Jumatatu, tarehe 9 Machi 2026, kufanya kazi za lazima ikiwemo kubeba mbao kwa ajili ya shughuli zao. Wakulima wanasema kwamba kazi hizo ziliwalazimishwa raia bila kujali umri, jambo lililoibua hasira katika jamii ya wenyeji.
Wananchi wanaona kwamba vitendo hivyo ni aina ya dhuluma dhidi ya watu ambao tayari wanakabiliwa na changamoto nyingi za kiusalama na kiuchumi. Wanasikitika kwamba hawa Wazalendo, ambao walitarajiwa kusaidia kulinda raia, sasa wanashutumiwa kwa kuwasumbua. Baadhi yao wanataka wapiganaji hao waondoke katika eneo hilo na mamlaka za serikali ziwapeleke FARDC ili kurejesha usalama.
Akizungumza kuhusu suala hilo, kiongozi wa eneo, Sikiryamuvha Vayunda, alithibitisha kuwepo kwa matukio hayo. Aliomba viongozi wa kiutawala na kiusalama katika ngazi zote wajihusishe haraka ili kupata suluhisho la kudumu na kuzuia matukio kama hayo kurudiwa.
Kwa kumbukumbu, Mikuha ni maeneo yaliyoko katika vijiji vya Bapakombe-Bakondo, wilaya ya Beni, mkoa wa Kivu Kaskazini, eneo ambalo kwa miaka mingi limekumbwa na hali tata ya kiusalama kutokana na uwepo wa makundi yenye silaha.
Obady Madirisha